Idara ya uhamiaji nchini imesema inawashikilia
wahamiaji haramu 2,048 kutoka nchi mbalimbali kwa tuhuma za
kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura.
Naibu
kamishna wa uhamiaji na msemaji mkuu wa idara hiyo, Abbas Mussa alisema
jana kuwa wahamiaji hao wanatoka nchi za Kenya, Burundi na Uganda.
Alisema
walikamatwa katika mikoa 14 wakijifanya ni Watanzania, lakini
ilibainika kuwa siyo raia baada ya idara hiyo kufanya uchunguzi kwenye
vituo vya uandikishaji.
“Baadhi yao tumewafikisha
mahakamani, lakini wengine bado uchunguzi unaendelea na wakibainika nao
watachukuliwa hatua,” alisema Mussa.
Aliongeza kuwa
wengi ya wahamiaji hao walifika mikoa ya Kagera, Mara, Tanga, Kigoma,
Rukwa, Kilimanjaro, Ruvuma, Geita, Shinyanga, Mtwara, Pwani, Mbeya,
Morogoro na Dar es Salaam.
“Inasikitisha sana, kwani baadhi ya waliokamatwa walishajiandikisha na kupewa vitambulisho kama raia wa Tanzania,” alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo, Idara imeamua kuongeza maofisa katika vituo ili kuendelea kuwabaini wahamiaji hao.
Mussa aliwataka wananchi kutoa taarifa mara wanapobaini watu ambao siyo raia wanajiandikisha.
Aliongeza
kuwa maombi ya hati za kusafiria yameongezeka maradufu kutoka hati
4,938 Julai 2014 hadi 8,703 Julai 2015 kwa upande wa Bara na kutoka hati
588 Julai 2014 hadi hati 1,028 Juni 2015 kwa upande wa Zanzibar.
Alisema
idara inawataarifu wananchi kuwa siyo lazima kubadilisha hati
inapokwisha muda wake, badala yake mmiliki anaweza kubadili na kupatiwa
nyingine wakati wowote atakapokuwa akisafiri.
No comments:
Post a Comment